MMOJA AFARIKI KATIKA MAANDAMANO  BRAZIL.
Raisi wa Brazil, Dilma 
Rousseff ameitisha mkutano wa dharura leo ikiwa ni siku moja baada ya 
muandamanaji kuuwawa na wengine zaidi ya milioni 1.25 wakiendelea 
kuandamana nchi nzima wakidai huduma nzuri kwa jamii. Pilikapilika
 hizo za uandamanaji ambazo mara nyingine zinaleta vurugu kubwa, 
zinafanyika wakati nchi hiyo iikiwa mwenyeji wa michuano ya Kombe la 
Shirikisho inayoendelea ambayo huchezwa mwaka mmoja kabla ya Kombe la 
Dunia. Raia wengi
 wa Brazil wamekuwa wakigadhabika juu ya gharama kubwa za maandalizi 
zilizotumika kwa ajili ya kuandaa na Kombe la Dunia 2014 na michuano ya 
olimpiki kipindi cha kiangazi itakayofanyika jijini Rio de Janeiro 2016.
  Jijini Rio 
polisi wamekuwa wakipambana na waandamanaji hao ambao hujikusanya karibu
 na Uwanja wa Maracana ambapo wamekuwa wakilazimika kutumia mabomu ya 
machozi na risasi za moto ili kuwatawanya.
 
PIRLO KUIKOSA BRAZIL.
Kiungo mahiri wa 
kimataifa wa Italia, Andrea Pirlo anatarajiwa kukosa mchezo wa mwisho wa
 kundi A dhidi ya wenyeji Brazil kwenye michuano ya Kombe la Shirikisho 
baada ya kupata majeraha ya msuli katika mguu wake wa kulia. Kocha
 wa viungo wa nchi hiyo, Enrico Castellacci amesema anamatumaini Pirlo 
anaweza kurejea katika mechi ya nusu fainali lakini ukijumuisha na 
kukosekana kwa Daniele De Rossi ambaye naye pia atakosa mchezo wa 
mwishoni itabidi kocha wa timu hiyo Cesar Prandelli abadili kikosi 
chake. Italia 
ilitinga hatua ya nusu fainali baada ya kuibugiza Japan ka mabao 4-3 na 
kufikisha alama sawa na Brazil katika kundi lao ambapo mechi ya mwisho 
ndio itakayoamua nani atasonga mbele kama mshindi wa kundi. Timu
 zote mbili itabidi zipange vikosi vyao kamili ili kutafuta ushindi na 
kuepuka kukutana na bingwa wa dunia Hispania katika hatua ya nusu 
fainali. 
HISPANIA WAPORWA HOTELINI WAKATI WAKIWA KWENYE MECHI.
Vyombo vya habari nchini
 Hispania vimeripoti kuwa wachezaji sita wa timu ya taifa ya Hispania 
wameibiwa fedha zao katika vyumba walivyofikia katika hoteli moja jijini
 Recife wakati wanacheza mchezo wao ufunguzi wa Kombe la Shirikisho 
dhidi ya Uruguay. Mojawapo
 ya wachezaji waliokumbwa na mkasa huo ni beki wa Barcelona, Gerard 
Pique ambaye aligundua kaibiwa wakati aliporejea chumbani kwake baada ya
 mchezo dhidi ya Uruguay ambao walishinda kwa mabao 2-1. Msemaji
 wa Shirikisho la Soka Dunia-FIFA, Pekka Odriozola alikiri kupata 
taarifa hizo lakini wameziachia mamlaka husika kushughulikia na kisha 
kuwaletea taarifa kamili. Hispania
 ambao wako kundi B jana wamefanikiwa kutinga hatua ya nusu fainali ya 
michuano hiyo kwa kishindi baada ya kuishindilia Tahiti kwa mabao 10-0 
wakati wawakilishi pekee wa Afrika kwenye mashindano hayo walishindwa 
kujihakikishia nafasi ya kusonga mbele baada ya kukubali kipigo cha 
mabao 2-1 kutoka kwa Uruguay.
MERCEDES WAFUNGIWA KUFANYA MAJARIBO MSIMU HUU.
Timu ya Marcedes 
imefungiwa kufanya majaribio kwa madereva wake chipukizi kwa mwaka huu 
pamoja na kupewa onyo kali kwa kosa la kufanyia majaribio magurudumu ya 
Pirelli kinyume cha utaratibu. Kampuni
 hiyo ya magurudumu ya Pirelli nayo pia imepewa onyo kwa kutumia gari 
jipya linalotumiwa katika mashindano ya langalanga na dereva Lewis 
Hamilton katika majaribio ya siku tatu waliyofanya nchini Hispania mwezi
 uliopita. Kamati
 maalumu ya uchunguzi wa suala hilo iliyoundwa na Chama cha Kimataifa 
cha Langalanga-FIA kilichukua hatua hiyo baada ya kuwakuta Mercedes na 
hatia ya kutenda kosa hilo ambalo ni kinyume cha utaratibu wa mashindano
 hayo. Katika 
sheria za langalanga timu yoyote hairuhusiwi kufanya majaribio 
magurudumu kwa zaidi ya kilometa 1000 pindi msimu wa mshindano hayo 
unapoanza na hata wakifanya majaribio hayo hawapaswi kutumia gari zao 
mpya zinazotumika katika msimu husika.
  
 
No comments:
Post a Comment