Pages

Friday, June 21, 2013

Habari za Michezo

MMOJA AFARIKI KATIKA MAANDAMANO  BRAZIL.

Raisi wa Brazil, Dilma Rousseff ameitisha mkutano wa dharura leo ikiwa ni siku moja baada ya muandamanaji kuuwawa na wengine zaidi ya milioni 1.25 wakiendelea kuandamana nchi nzima wakidai huduma nzuri kwa jamii. Pilikapilika hizo za uandamanaji ambazo mara nyingine zinaleta vurugu kubwa, zinafanyika wakati nchi hiyo iikiwa mwenyeji wa michuano ya Kombe la Shirikisho inayoendelea ambayo huchezwa mwaka mmoja kabla ya Kombe la Dunia. Raia wengi wa Brazil wamekuwa wakigadhabika juu ya gharama kubwa za maandalizi zilizotumika kwa ajili ya kuandaa na Kombe la Dunia 2014 na michuano ya olimpiki kipindi cha kiangazi itakayofanyika jijini Rio de Janeiro 2016.  Jijini Rio polisi wamekuwa wakipambana na waandamanaji hao ambao hujikusanya karibu na Uwanja wa Maracana ambapo wamekuwa wakilazimika kutumia mabomu ya machozi na risasi za moto ili kuwatawanya.
 

PIRLO KUIKOSA BRAZIL.

Kiungo mahiri wa kimataifa wa Italia, Andrea Pirlo anatarajiwa kukosa mchezo wa mwisho wa kundi A dhidi ya wenyeji Brazil kwenye michuano ya Kombe la Shirikisho baada ya kupata majeraha ya msuli katika mguu wake wa kulia. Kocha wa viungo wa nchi hiyo, Enrico Castellacci amesema anamatumaini Pirlo anaweza kurejea katika mechi ya nusu fainali lakini ukijumuisha na kukosekana kwa Daniele De Rossi ambaye naye pia atakosa mchezo wa mwishoni itabidi kocha wa timu hiyo Cesar Prandelli abadili kikosi chake. Italia ilitinga hatua ya nusu fainali baada ya kuibugiza Japan ka mabao 4-3 na kufikisha alama sawa na Brazil katika kundi lao ambapo mechi ya mwisho ndio itakayoamua nani atasonga mbele kama mshindi wa kundi. Timu zote mbili itabidi zipange vikosi vyao kamili ili kutafuta ushindi na kuepuka kukutana na bingwa wa dunia Hispania katika hatua ya nusu fainali.

HISPANIA WAPORWA HOTELINI WAKATI WAKIWA KWENYE MECHI.

Vyombo vya habari nchini Hispania vimeripoti kuwa wachezaji sita wa timu ya taifa ya Hispania wameibiwa fedha zao katika vyumba walivyofikia katika hoteli moja jijini Recife wakati wanacheza mchezo wao ufunguzi wa Kombe la Shirikisho dhidi ya Uruguay. Mojawapo ya wachezaji waliokumbwa na mkasa huo ni beki wa Barcelona, Gerard Pique ambaye aligundua kaibiwa wakati aliporejea chumbani kwake baada ya mchezo dhidi ya Uruguay ambao walishinda kwa mabao 2-1. Msemaji wa Shirikisho la Soka Dunia-FIFA, Pekka Odriozola alikiri kupata taarifa hizo lakini wameziachia mamlaka husika kushughulikia na kisha kuwaletea taarifa kamili. Hispania ambao wako kundi B jana wamefanikiwa kutinga hatua ya nusu fainali ya michuano hiyo kwa kishindi baada ya kuishindilia Tahiti kwa mabao 10-0 wakati wawakilishi pekee wa Afrika kwenye mashindano hayo walishindwa kujihakikishia nafasi ya kusonga mbele baada ya kukubali kipigo cha mabao 2-1 kutoka kwa Uruguay.

MERCEDES WAFUNGIWA KUFANYA MAJARIBO MSIMU HUU.

Timu ya Marcedes imefungiwa kufanya majaribio kwa madereva wake chipukizi kwa mwaka huu pamoja na kupewa onyo kali kwa kosa la kufanyia majaribio magurudumu ya Pirelli kinyume cha utaratibu. Kampuni hiyo ya magurudumu ya Pirelli nayo pia imepewa onyo kwa kutumia gari jipya linalotumiwa katika mashindano ya langalanga na dereva Lewis Hamilton katika majaribio ya siku tatu waliyofanya nchini Hispania mwezi uliopita. Kamati maalumu ya uchunguzi wa suala hilo iliyoundwa na Chama cha Kimataifa cha Langalanga-FIA kilichukua hatua hiyo baada ya kuwakuta Mercedes na hatia ya kutenda kosa hilo ambalo ni kinyume cha utaratibu wa mashindano hayo. Katika sheria za langalanga timu yoyote hairuhusiwi kufanya majaribio magurudumu kwa zaidi ya kilometa 1000 pindi msimu wa mshindano hayo unapoanza na hata wakifanya majaribio hayo hawapaswi kutumia gari zao mpya zinazotumika katika msimu husika.
 

No comments:

Post a Comment