Rais Jakaya Kikwete 
            
    Dar/Dodoma. Rasimu ya Katiba Mpya iliyozinduliwa jana, imependekeza kupunguzwa kwa madaraka ya Rais wa Tanzania maeneo tofauti ya utendaji wake, ukiwamo uteuzi wa viongozi na watendaji wakuu wa Serikali.
Tume hiyo inapendekeza kwamba Rais ashirikiane na 
mihimili mingine ya dola katika uteuzi huo, huku ikiwataja Mawaziri na 
Naibu Mawaziri, Jaji Mkuu, Naibu Jaji Mkuu na Katibu Mkuu Kiongozi kuwa 
uteuzi wao utakapofanywa na Rais lazima uthibitishwe na Bunge.
Mapendekezo hayo ni tofauti na hali ilivyo sasa 
wakati uteuzi unaofanywa na Rais hauthibitishwi na Bunge, isipokuwa 
nafasi ya Waziri Mkuu na Makamu wa Rais itapotokea ikawa wazi kwa sababu
 zozote zile.
Pia, tume inapendekeza Rais ashauriane na chombo 
kipya kitakachoundwa cha Baraza la Ulinzi la Taifa kuwateua viongozi 
wote wa taasisi za ulinzi nchini.
Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji 
Joseph Warioba alisema mfumo wa utawala utaendelea kuwa kama ulivyo hivi
 sasa na kwamba, Rais ndiye mtendaji wa Jamhuri ya Muungano na 
atachaguliwa moja kwa moja na wananchi.
Jaji Warioba alisema Tume imependekeza mgombea 
urais lazima apate zaidi ya asilimia 50 ya kura zilizopigwa na kwamba, 
kinga ya kutokuhoji matokeo ya uchaguzi mahakamani iondolewe.
“Mgombea urais anaweza kupendekezwa na chama cha 
siasa au kuwa mgombea huru, mgombea wa nafasi hiyo atatangazwa kuwa 
mshindi iwapo atakuwa amepata zaidi ya asilimia 50 ya kura zote 
zilizopigwa,” alisema Jaji Warioba na kuongeza: “Hata hivyo, matokeo ya 
uchaguzi wa Rais yanaweza kulalamikiwa mahakamani, lakini siyo kila mtu 
anaweza kufungua kesi, wanaoweza kufungua kesi ni wagombea urais na 
Mahakama ya Juu pekee ndiyo itakuwa na mamlaka na uwezo wa kusikiliza 
malalamiko kuhusu matokeo ya uchaguzi wa Rais na shauri lazima liamuliwe
 ndani ya mwezi mmoja, yaani siku 30.”
Alisema Tume inapendekeza Rais achaguliwe moja kwa moja na wananchi na kwamba, suala la umri pia lilijadiliwa kwa upana.
“Wengine walisema umri wa mtu kuruhusiwa kugombea 
urais uwe miaka 35 au 50 na kuendelea, Tume imeyachambua maoni yote na 
ikafanya utafiti kwa kupitia Katiba za nchi zingine ,” alisema Jaji 
Warioba na kuongeza:
“Wengi walioomba kugombea nafasi hiyo walikuwa na 
umri wa miaka 40 au zaidi, kwa kuzingatia maoni ya wananchi, utafiti na 
hali halisi, Tume imependekeza Rais aendelee kuchaguliwa na wananchi 
pamoja na sifa nyingine mtu atakayegombea Urais asiwe chini ya miaka 
40.”
Kutokupunguzwa kwa umri wa urais kutakuwa ni pigo 
kwa wansiasa vijana nchini waliopendekeza ushushwe na kuwa miaka 35, 
akiwamo Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe na Naibu Waziri wa 
Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Januari Makamba.
Zitto, Makamba watoa kauli.
Akizungumzia suala hilo jana, Zitto alisema uamuzi huo wa umri 
hana la kusema, kwa sababu yaliyotolewa ni mapendekezo ya Tume na 
kwamba, Chadema watatoa kauli baada ya viongozi kuwasiliana.
Kwa upande wake, Makamba iwapo amebadili msimamo wake, alisema: “Suala la umri siyo kigezo pekee cha kupata uongozi mzuri.”
Makamba alisema ujana wala uzee siyo kigezo cha kumnyima mtu uongozi.
Siku za nyuma Makamba, ambaye ni Mbunge wa 
Bumbuli, aliwahi kunukuliwa akitaka umri wa kugombea urais uwe miaka 35 
badala ya 40 ya sasa.
Alisema suala la umri lisingemwathiri binafsi, kwani mwaka 2015 atakuwa na umri wa miaka 41.
“Ninapongeza Watanzania kwa kutoa maoni yao na kutaka vijana kupewa nafasi za uongozi,” aliongeza Makamba.
No comments:
Post a Comment